03 December 2013

KIM AWAFURAHIA SAMATTA, ULIMWENGU


  • SASA KUIVAA BURUNDI KESHO

 Na Mwandishi Wetu, Nairobi
 Kocha Mkuu wa timu ya Taifa ya Tanzania Bara, Kilimanjaro Stars, Kim Poulsen amesema kwamba kuwasili katika kikosi chake kwa wachezaji Thomas Ulimwengu na Mbwana Samatta kutaongeza nguvu katika kikosi hicho hasa katika mchezo wao wa kesho wa Kombe la Challenji dhidi ya Burundi

Samatta na Ulimwengu waliwasili jijini Nairobi wakitokea kuichezea timu yao, TP Mazembe ya DRC katika Fainali ya Kombe la Shirikisho Afrika, ambayo walifungwa jumla ya mabao 3-2 na timu ya CS Sfaxien ya Tunisia na hivyo kukosa kombe.

Akizungumza jijini Nairobi jana, Kim alisema ujio wa wachezaji hao ni ahueni katika kikosi chake ambacho bado kinakabiliwa na mechi ngumu dhidi ya Burundi kwani aliiona timu hiyo na anaimani italeta upinzani mkali.

"Wachezaji nilionao ni wazuri lakini kuongezeka kwa Samatta na Ulimwengu pia kumeongeza nguvu zaidi katika kikosi changu, hivyo nategemea mechi ya Jumatano itakuwa nzuri zaidi," alisema kocha huyo.

Alisema timu zote zinazoshiriki michuano hiyo hakuna timu kibonde, hivyo hata wakivuka robo fainali bado watakuwa na kazi ngumu katika kuhakikisha wanatwaa kombe hilo na kurudi nalo Tanzania.

Kim alisema anaendelea na mazoezi katika kuboresha kikosi chake, kwani kuna mapungufu ambayo aliyagundua walipocheza na Somalia, hivyo anatakiwa kuyafanyia kazi haraka kabla ya mechi yao ya kesho.

Stars imeambulia pointi nne na mabao mawili baada ya kutoa sare ya bao 1-1 na Zambia katika mchezo wa kwanza na ushindi wa 1-0 dhidi ya timu dhaifu, Somalia juzi.

No comments:

Post a Comment